Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Rhimo Nyansaho, amewataka vijana wanaopata mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kutumia stadi wanazozipata kujiajiri, kujitegemea na kuwa raia wema.
Akiwasilisha bajeti ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma leo Mei 19, 2026, Dkt. Nyansaho amesema mafunzo ya JKT yameendelea kuwajengea vijana uzalendo, ukakamavu, umoja wa kitaifa pamoja na stadi mbalimbali za maisha na kazi.
“Nitoe rai kwa vijana wote wanaopata fursa ya mafunzo hayo kuwa raia wema na kuzitumia stadi walizozipata kujiajiri na kujitegemea,” amesema Dkt. Nyansaho.
Aidha, amesema Serikali inaendelea kuboresha miundombinu ya kambi za JKT ambapo hadi mwaka wa fedha 2025/2026 kambi hizo zilikuwa na uwezo wa kuchukua zaidi ya vijana 60,000.
Kwa mujibu wa Waziri huyo, mpango uliopo ni kuendelea kufungua kambi mpya na kuboresha zilizopo ili JKT iweze kuchukua vijana 140,000 ifikapo mwaka 2031.
Mafunzo hayo hufanyika katika makundi mawili ambayo ni Kundi la Kujitolea na Kundi la Lazima kwa vijana wanaohitimu Kidato cha Sita katika kambi mbalimbali za JKT.

Post a Comment