Waziri Mbarawa Atoa Neno Uwanja Wa Ndege Msalato Dodoma

 Na Mwandishi Wetu


WAZIRI wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kwa ujasiri na uwezo mkubwa katika kusimamia miundombinu ikiwemo ujenzi wa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Msalato Dodoma



Alisema hayo wakati alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo


“Tunamshukuru sana Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa ni mjasiri na uwezo mkubwa katika kusimamia miundombinu, Wizara ya Uchukuzi tunamshukuru sana, leo tumesimama katika lami ya kiwanja cha ndege cha Msalato,” alisema


 


Aliwataka wakandarasi kujipanga ili mradi ukamilike kwa wakati.


“Hakuna shida ya fedha, fedha zipo mkandarasi atoe certificate ili tuweze kumlipa lakini kuna changamoto za mvua ni vyema mkatengeneza mpango kazi kuhakikisha mradi unakamilika kama ulivyopangwa Mei mwakani,” alisema


Alisema kuwa ujenzi umekamilika kwa asilimia 47 upande wa miundombinu mradi umekamilika kwa asilimia 12.4 upande wa majengo.



Alisema kuwa mradi huo unajengwa kwa thamani ya Sh  bilioni 354, kati ya hizo Sh bilioni 164  kwa ajili ya njia ya kutokea ndege ,maegesho , kuingilia ndege na Sh bilioni 194 kwa ajili ya jengo la abiria.


Alisema kuwa uwanja huo ni mkubwa utakuwa na kilomita 3.6.


“Utakuwa na sifa za pekee ya kuwa na vifaa vya kisasa vya kuongozea ndege, mfumo wa kuruhusu ndege kutua masaa 24 kuwe na mvua ,jua au ukungu ndege itatua tofauti na viwanja vingine,


Pia uwanja huo utaweza kuchukua ndege kubwa kama aina ya Air bus.


Alisema kwa upande wa majengo, jengo litakuwa na uwezo wa kuchukua abiria milioni 1.5 kwa mwaka, na kutakuwa na mfumo wa kuongozea ndege wenye urefu wa mita 56 sawa na ghorofa 16.3, utakuwa ni uwanja mzuri na wa kisasa.


Kwa upande wake, Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Zuhura Amani alisema kuwa katika utekelezaji wa mradi wa miundombinu mradi  utakuwa na maegesho ya magari 500, uzio ukubwa wa kilomita 37 mradi ulisainiwa Septemba 2022,kwa gharama ya Sh  bilioni 165.6  mkataba wa miezi 36 mradi ulianza Aprili 2022 na utakamilika Aprli 2025.


Pia alisema  utekelezaji wa mradi wa miundombinu umefikia asilimia 47.9, mradi umeajiri wafanyakazi 495 kati ya hao 464 ni Watanzania.


Alisema mradi wa majengo utahusisha ujenzi wa jengo la abiria lenye uwezo wa kuhudumia abiria milioni 1.5 kwa mwaka,ujenzi wa jengo la kuongoza ndege, usimikaji wa vifaa vya mfumo wa kuongozea ndege, ujenzi wa jengo la zimamoto, lenye uwezo wa kuhudumia ndege daraja la 4E na mifumo wa kuongozea ndege,  kituo cha kufua umemne, jengo la hali ya hewa na usimikaji wa mitambo yake.


Alisema mkandarasi amesaini mkataba kwa gharama ya Sh bilioni 194.4 bila ongezeko la kodi , mkataba ulianza Novemba 2022, utakamilika Novemba 2025, utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 12.4, ambapo kuna jumla ya wafanyakazi 389  kati ya hao 359 ni Watanzania.


Alisema kuwa mradi huo unafadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB)


Alisema kuwa jumla ya wananchi 1,772 walilipwa kiasi cha Sh bilioni  14.9 kama fidia ya kupisha eneo hilo.


 Alisema kuwa kumekuwwepo na changamoto ya mvua katika utekelezaji wa mradi lakini wameweka mikakati kuhakikisha mradi unakamilika kama ilivyopangwa.


Kwa upande wake Katibu Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Dodoma Jawadu Mohamed alisema kuwa ilani ya CCCM imekuwa ikitekelezwa kwa vitendo katika mkoa wa Dodoma.


Alisema kuwa wakati Rais Samia aliiingia madarakani wengi walikuwa na mashaka juu ya ukamilishwaji wa miradi ikiwemo Mji wa Serikali, barabara za mzunguko na uwanja wa ndege wa kimataifa wa Msalato Dodoma.


“Rais Samia amepambana kuhakikisha akakamilisha kazi hizo, tumuunge mkono kiongozi huyu wan chi kwenye jitihada kubwa anazofanya,” alisema


Mkuu wa Wilaya ya Kondoa Dk Hamisi Mkanachi, ambaye alimwakilisha mkuu wa mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule aliwataka wakandarasi hao kuongeza nguvu, ikiwemo nguvu kazi ili mradi huo ukamilike  kwa wakati.

Post a Comment

Previous Post Next Post