NA PAUL KAYANDA- KAHAMA.
WAKATI Waziri wa Ardhi Nyumba na Maenedeleo ya Makazi Jery Silaa akikemea watendaji wa Wizara hiyo pamoja na Viongozi wa Chama na Serikali kutokuwa chanzo cha Migogoro,baadhi ya Viongozi wa Chama cha Mapinduzi na Serikali ngazi ya Kitongoji na Kata ya Mhungula Manispaa ya Kahama wanalalamikiwa kuuza eneo la Rose Sylivester mkazi wa Kahama Mkoani Shinyanga.
Viongozi hao wanalalamikiwa kwa kujihusisha na Mtandao hatari wa kuuza maeneo ya watu mbalimbali huku wakitumia kivuli cha Uongozi na Madaraka waliyo nayo kupokea Rushwa na kupindisha Haki za watu.
Sema Media imepata nakala ya barua ya tarehe 15.02 2023 iliyoandikwa na Rose Sylivester kwenda kwa Ofisa Mtendaji wa Kata ya Mhungula akimweleza kuwa hana Imani na Baraza la Kata pamoja na Ofisi ya Serikali ya Mtaa ya Inyanga Kata ya Mhungula.
Bi Rose analalamikia kitendo cha Baraza la Ardhi kupelekewa malalamiko ya kuvamiwa kwa shamba lake lenye ukubwa wa Ekari 16 lililopo Mtaa wa Inyanga Kata ya Mhungula katika Shauri la Madai Na 7/2021 ambapo Rosemary alishinda katika Shauri hilo lakini baraza hilo limeshindwa kuheshimu maamuzi yake.
Baada ya uvamizi huo Bi Rose alipeleka malalamiko yake katika Ofisi ya Serikali ya Mtaa wa Inyanga kuomba kibali cha kupimiwa eneo ambapo alipatiwa na alipokwenda Idara ya Ardhi alikabidhiwa kwa Ofisa upimaji wa Ardhi (Land Surveyor)ilia je kumpimia.
Bi Rose Sylivester anasema baada ya kuonana na Mwenyekiti wa baraza la Ardhi la Kata pamoja na Ofisa Mtendaji wa Mtaa walikataa kumpa ushirikiano na kumweleza Ofisa upimaji huyo kwamba eneo hilo lina Mgogoro.
Mwenyekiti wa baraza la Ardhi la Kata ya Mhungula pia anadaiwa kukataa kumpa ushirikiano Ofisa upimaji huyo akimweleza kuwa katika eneo hilo kuna wamiliki wengine halali wa eneo hilo wakati siyo kweli huku ikidaiwa kuwa anafanya vitendo hivyo kutokana na kutafuta kupatiwa Rushwa.
Kwa mujibu wa Rose,pamoja na kuwepo kwa madai hayo yaliyotolewa na Mwenyekiti kwa Ofisa Ardhi watu wanaodaiwa kuwa na viwanja katika eneo lake hakuna mtu hata mmoja aliyewahi kumpelekea barua ya wito wala akimlalamikia mahala popote.
Katika kuthibitisha njama za Mwenyekiti huyo kutengeneza mazingira ya Rushwa,ni pale inapofikia anatengeneza Kesi na kuisikiliza upande mmoja bila mlalamikiwa kujulishwa na kumaliza Kesi kwa kumpa ushindi mlalamikaji jambo ambalo ni matumizi mabaya ya madaraka.
Katika hatua nyingine Mwenyekiti wa Baraza la Kata ya Mhungula anadaiwa kutengeneza kikundi cha waandamanaji wapatao 36 wakiwa na Silaha za jadi na kuwapeleka shambani kwa Bi Rose kwa lengo la kugawiwa Viwanja.
“Mimi nilipata taarifa hizo kutoka kwa msamaria mwema akiniambia kuwa Shambani kwako kuna watu ambao wameambatana na Mwenyekiti wa baraza la Kata akiambatana na Viongozi wa Ofisi ya Serikali ya Mtaa wa Inyanga”alisema Bi Rose Sylivester.
Hata hivyo Bi Rose Silvester,anasema Kesi ya Msingi katika eneo hilo iliisha tangu mwaka 2021 ambapo kwa mujibu wa baraza hilo lilisema limejiridhisha kuwa Shamba hilo ni mali yeke.(Nakala tunayo)
“Mwaka 2021 nililalamikia kuvamiwa kwa eneo langu lenye ukubwa wa Ekari 16 baraza likafanya uchunguzi kwa kuhoji mashahidi wangu pamoja na mashahidi wa mlalamikaji na kujiridhisha kuwa Shamba hilo ni mali yangu na kusisitiza kuwa Shamba hilo lisiingiliwe wala kupokonywa na mtu yeyote,sasa hapo kuna kesi gani tena?”alihoji Bi Rose Sylivester.
Kutokana na vitendo vinavyofanywa na Viongozi wa Chama waliochaguliwa na wananchi ili kuwaongoza na kuendekeza Migogoro ya Ardhi badala ya kutenda Haki Bi Rose Sylivester amemuomba Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Jery Silaa kufanya Ziara kuja katika Manispaa ya Kahama ili kuja kujionea namna wananchi wanyonge wanavyofanyiwa vitendo vya hovyo na Viongozi wa wao waliowachagua.
Taarifa za ndani ambazo gazeti hili limezipata kutoka ndani ya Ofisi ya Mwenyekiti wa Mtaa wa Inyanga Nestory Bugomola zimebainisha bila ubishi kwamba,eneo linalobishaniwa ni mali ya Rose Sylivester kutokana na historia ya asili.
“tukiacha unafiki na kuendekeza uchochezi wa Migogoro ya Ardhi katika Jamii,ukweli kuhusiana na nani ndiye mmiliki halali wa eneo hilo,mimi naomba kuwa muwazi,eneo hilo ni mali ya Rose Sylivester”alisema Rose.
Sema Media ilimtafuta mmoja wa Wenyeviti wa Vitongoji ili kupata maoni ya kilichosababisha kushamiri kwa Migogoro katika Manispaa ya Kahama ambapo Mwenyekiti huyo alisema chanzo cha kushamiri kwa Migogoro ni kutokana na tama ya Viongozi waliochaguliwa kwa ajili ya kuwawakilisha wananchi.
“kushamiri kwa Migogoro katika Manispaa ya Kahama ni kutokana na tamaa ya sisi Viongozi wa kuchaguliwa na wananchi,utakuta Mwenyekiti anashawishiwa kwa fedha aandike Mikataba mipya baada ya mtu kudanganya kuwa nyaraka za awali zilipotea na hapo kinatumika kishawishi cha nguvu ya fedha”alisema Mwenyekiti huyo ambaye hakupenda jina lake liandikwe kwa ajili ya kiusalama.
Mwenyekiti wa Mtaa wa Inyanga Nestory Bugomola alipotafutwa kuzungumzia tuhuma za kudaiwa kuuza maeneo ya wananchi alikana kuwa sehemu ya viongozi wanaotuhumiwa kuuza maeneo ya watu badala yake amewataka wananchi kuacha kuvamia maeneo ya watu,na kuwataka kutafuta maeneo kwa kufuata Sheria na kanuni zilizowekwa na Serikali.
“Mimi siyo sehemu ya viongozi wanaouza maeneo ya watu na katika nyaraka hizo sidhani kama mmeshuhudia Sahihi yangu katika nyaraka hizo niwaombe wananchi waache kuvamia maeneo ya watu, wafuate Sheria na kanuni zilizowekwa na Serikali”alisema Bugomola.




Post a Comment